Shukrani zilizo takasika ni zake Allah (s.w.t) asiyekuwa na mshirika katika Ibada yake wala katika ufalme wake.
Rehema na Amani zishuke juu ya Mtume Muhammad (s.a.w) na wale wote wenye kushikamana naye.
Mwenyezi Mungu ametujaalia wanadamu kuwa makundi mbali mbali kama vile masikini na matajiri, wafanyakazi na wakulima na makundi mengine mengi. Pamoja na kuwepo na makundi mbali mbali kila kundi linatakiwa kumcha Allah (s.w.t) na kuwa mstari wa mbele katika kuendeleza dini.
Wewe na mimi tumetamka shahada mbili na tumekiri katika nyoyo zetu kuwa mwenye jina la Allah ndiye Mungu wa kweli na Muhammad ni Mtume wake, Kukiri na kutamka shahada ni dalili tu ya kujulisha kuwa sisi ni waislamu. Ili uislamu wetu uweze kukamilika tunatakiwa kuyafanya yale ambayo wametuagiza Allah (s.w.t.) na Mtume wake (s.a.w) na kuyaacha yale ambayo wametukakaza.
Katika makundi tuliyonayo wanadamu, kundi la wafanya kazi huwa wamepitia hatua mbalimbali kama vile shule ya msingi, sekondari, chuoni na hatimaye kazini. Sasa ewe uliyejaaliwa kuajiriwa ujiulize ukiwa shule ya msingi, sekondari na chuoni, mlianza wangapi, mlifaulu wangapi na mpaka hivi sasa ni wangapi mnaendelea na kazi?
Je, wale ambao hawakufanikiwa katika yale maeneo ambayo wewe umefanikiwa unafikiri ni uzembe wao au Allah hakuwawezesha? Na wewe uliyefanikiwa unafikiri umefanikiwa kwa ujanja wako au Allah ndiye aliyekuwezesha?
Allah (s.w.t) humpa amtakaye na humnyima amtakaye, umekuwa miongoni mwa waliopewa na Allah basi nawe utoe katika njia ya Allah ili kuendeleza dini yake si kwaajili ya kumnufaisha mwenyezi mungu bali ni kwaajili ya kutaka radhi ili aendelee kukuruzuku na kulinda mali yako.
Mwenyezi Mungu anatuhimiza kwa kusema ndani ya Quran: ENYI MLIOAMINI TOENI KATIKA VILE TULIVYOKUPENI KABLA HAIJAFIKA SIKU AMBAYO HAPATAKUWA (NA) KUJIKOMBOA WALA URAFIKI (WA KUSAIDIANA) WALA UOMBEZI, NA WALIOKUFURU NDIO WALIO JIDHULUMU (KWELIKWELI) Q:2:254.
Allah (s.w.t.) ametuumba wanadamu akatupa uwezo kuliko viumbe wote, ametupa elimu, akatupa pia uhuru wa kuweza kupanga na kupangua, kutanda na kutandua, kufunga na kufungua na mengine mengi. Tujiulize enyi wenzangu, katika kipato chetu tunatumia kiasi gani katika mambo ya anasa?
Kwanini tunakunja mikono yetu katika upande wa kundeleza dini yetu?
Sisi tuliojaaliwa kuwa na uhakika wa kipato tena kwa muda maalumu tunakuwa wazito kutoa. Je, wale wasio kuwa na uhakika wa kipato kwa muda maalumu wataweza? Waislamu wenyewe tusipo iendeleza dini yetu asiye kuwa Muislamu ataweza kuundeleza Uislamu?
Allah (s.w.t) amemsifu binaadamu kwa kusema “ HAKIKA TUMEMUUMBA MWANAADAMU KATIKA UMBO LILILO BORA KABISA”Q 95:4. Hapa inamaana wewe na mimi tumejaliwa vipawa vinavyoweza kutuwezesha kutambua dhima ya kuumbwa kwetu na hatima ya maisha yetu hapa duniani na kesho akhera.
Enyi ndugu zangu katika imani na dinI tujitahidi kutoa bila kuwa na mashaka ya kulipwa katika vile tunavyovitoa, Allah ameahidi kumlipa kila mtu kwa kila akifanyacho kiwe cha kheri au shari, kidogo au kikubwa, akiwa ametoa kwa siri au wazi kama anavyosema ndani ya Quran 2:274 “WALE WANAOTOA MALI ZAO USIKU NA MCHANA KWA SIRI NA DHAHIRI, WANAUJIRA WAO KWA MOLA WAO, WALA HAITAKUWA KHOFU JUU YAO WALA HAWATAHUZUNIKA”
Ewe Mwenyezi Mungu , kila atakaye kunjua mkono wake na kutoa kwako basi mtengenezee mambo yake hapa Duniani na Kesho Akhera.