Wednesday, May 2, 2012


NAWASHUKURU KWA KUNICHAGUA KUWA MBUNGE WA B.A GENERAL
Kila sifa njema ni zake Allah  (S.W) ambaye atakapo jambo husema kuwa na likawa, Rehema na Amani zishuke juu ya kipenzi chake na chetu pia Muhammad (s.a.w) na wafuasi wake wote.
Napenda kutumia nafasi hii kuwashukuru wote walionipigia kura na wasionipigia kura. Walionipigia kura ninawashukuru kwani wameonesha imani yao kwangu na wanaamini kuwa ninaweza kukifanya kile watakachohitajia. Wasionipigia kura nao sinabudi kuwashukuru kwani ni changamoto kwangu isije nikabweteka kwa kujiona kuwa ninaweza kumbe ninatakiwa kuongeza juhudi ili niweze zaidi.
Mawakala wangu, wagombea wenzangu na wote waliosimamia zoezi la uchaguzi nao siwezi kuwasahau kwani walikuwa tayari kuhakikisha wanasimamia zoezi kwa hatua zote , namuomba mwenyezi Mungu awalipe kila la kheri kwa uadilifu wao.
Ndugu zangu nashukuru kwa kuniamini kwenu na kunipa dhamana kubwa, dhama mliyonipa nitajitahidi kadri ya uwezo wangu kuhakikisha ninaifanya kwa nguvu zangu zote, lakini kikubwa ninachowaombeni ni dua zenu kwani bila msada wa Mwenyezi Mungu siwezi kufanya lolote lile.
Pia litakuwa si jambo la kiungwana kama nitawasahau kuwashukuru wale ambao hawajapiga kura na wale walioharibu kura zao. Makundi haya mawili ninaamini wapo waliochukua maamuzi yao kutokana na fikra, imani na mitazamo yao, lakini wapo waliosukumwa na marafiki. Hawa waliosukumwa na marafiki tunaweza kusema wanafanya mambo KIBUBUSA yaani wanafuata mkumbo. Kufanya jambo KIBUBUSA kwa msomi tena wa chuo kikuu ni jambo linaloweza kushangaza jamii, kwani jamii inaamini kuwa msomi ndio kiigizo chema na ni chanzo cha fikra na maamuzi sahihi. Hapa tatizo si maamuzi bali tatizo ni kufanya jambo kwa kufuata maamuzi ya mtu fulani  pasina ya kujua kuwa wewe mwenyewe unatakiwa uwe na sababu, fikra, mtazamo, haja na uwe ndio chanzo cha maamuzi.
Katika tasinia ya siasa kuchafuana na kupakana matope limekuwa ni jambo linaloonekana kuwa ni la kawaida. Nasi katika mchakato wetu wa uchaguzi wapo walioeneza sifa zisizo zangu wengine walinichafua ili nikataliwe. Hawa wote sinabudi kuwashukuru kwani maneno na mapambo yao yalikuwa ni ufunguo wa kuwafanya wapiga kura wafanye udadisi juu yangu na kupata ukweli na hatimaye wakafanya maamuzi sahihi.
Muda hautoshi na nafasi ni ndogo wako wengi wakushukuriwa kikubwa niseme tu kila mmoja kwa nafasi yake ninamshukuru, na ninaendelea kuwaombeni mniombee kwa Allah ili niweze kufanya kile kinachomridhisha yeye na kile ambacho ninyi pia kitawaridhisha kumbukeni kuwa “HAYA TULIYONAYO NDIO MAISHA YENYEWE, HAKUNA MAISHA MENGINE ZAIDI YA HAYA KWA HAPA DUNIANI.
Kiongozi ni kama KIRAKA katika nguo. Kiongozi makini ni kama KIRAKA katika nguo iliotoboka na kiongozi mbovu ni kama KIRAKA katika nguo isiyotoboka. KIRAKA katika nguo iliyotoboka kina kazi ya kufanya, nayo ni kusitiri sehemu iliyowazi na KIRAKA katika nguo isiyotoboka hakina kazi ya kufanya ingawa utaniambia ni pambo. Tangu enzi za wahenga hadi leo KIRAKA hutumika kwa kuziba sehemu iliyowazi na wala si pambo kama usemavyo wewe. Ni matumaini yangu kuwa wote tuliochaguliwa kwa kushirikiana nanyi mliotuchagua kwa msaada wake Allah tutafanya mambo yatakayo tuwezesha kupata mafanikio hapa Duniani na kesho Akhera.
Ndimi:  FAKIHI S. MSHAMU  (MWL/Dr. NAHONYO)