Kila
sifa njema ni zake Mwenyezi Mungu
aliyemuumba Mwanadamu katika umbo bora.
Watanzania wenzangu, uchaguzi unapokaribia, wagombea huonekana wapole,
wakarimu, wenye kauli zenye matumaini na wenye kuwajali wananchi. Kabla na
baada ya uchaguzi ukali, majivuno, dharau na ubabe kwa wananchi huwa ndio
kawaida yao.
Leo si ajabu kuwaona
wagombea wakigawa fedha, nguo na vitu vingine bila hata kuombwa. Tunawapongeza
kwa moyo wao wa kutoa lakini wanatakiwa watupe majibu kwa nini misaada yao ije
wakati huu wa uchaguzi na si kabla ya hapo? Vitu hivi ni nini kama si RUSHWA?
Watanzania wenzangu, hivi tuko tayari kuuza ukristo na uislamu wetu? Dini zetu
zinatuonya juu ya kutoa na kupokea RUSHWA. Uislamu, mtume Muhammadi (S.a. w) anasema
“Mwenyezimungu amemlaani mtoa Rushwa,mpokea Rushwa na anayewaunganisha wawili
hawa”. Katika Qur’ani Mwenyezimungu anasema”NA UTAWAONA WENGI KATIKA WAO
WANAKIMBILIA KATIKA DHAMBI NA UADUI NA ULAJI WAO WA HARAMU. BILA SHAKA
WAYAFANYAYO HAYO NI MABAYA KABISA (Q 5:62)” Ndani ya Bibilia nako wakristo
wamekemewa vibaya”. KWELI JEURI HUMPUMBAZA MWENYE HEKIMA, NA RUSHWA HUHARIBU
UFAHAMU (MHUBIRI:7:7).
Watanzania wenzangu RUSHWA
ni kipimo cha kumtambua kiongozi bora na asiyebora. Kama mgombea akikujia
kukuomba kura yako na kukupa kitu kidogo ujue wazi kuwa huyo amepoteza sifa ya
kuwa kiongozi, ukimchagua kiongozi kwa sababu tu ametoa RUSHWA ujue kuwa ni
kumpa meno yatakayo mjengea dharau na majivuno juu yako. Akichaguliwa kwa njia
ya RUSHWA kiongozi hujiona pesa zake ndizo zilizomchagua na si wewe mtanzania
mwenzangu uliyempigia kura.
Leo ukitangaza nia ya
kugombea nafasi fulani watu watakuuliza “unapesa?”. Tabia hii ndiyo
inayopelekea tupate viongozi wabovu ati kwa sababu tu wanapesa, asiyekuwa na
pesa hata kama anasifa njema watu
hawamjali. Naikumbusha nafsi yangu na yako ewe uliyejaliwa akili timamu, RUSHWA
ni adui katika jamii, Serikalini na katika dini, tujilazimishe kuikataa ili
tusichague PUMBA tukaacha MCHELE.
Poleni watanzania wenzangu
mnaodanganyika kwa sasa mkawa tayari
kupokea RUSHWA na kujiingiza katika upofu wa maamuzi. Ombi langu kwenu
mchagueni kiongozi bora na si bora kiongozi, hata kama mtu amewajieni kwa
baiskeli lakini akawa na hoja thabiti zinazoonesha matumaini mchangueni
atawafaeni kuliko huyo mtoa RUSHWA.
FAKIHI S. MSHAMU (MWL NAHONYO).
SIMU: 0784950236/0712829903.
Blog:www.nahonyo.blogspot.com.
MFAHAMU
FAKIHI MSHAMU (MWL NAHONYO).
Huyu
ni mwalimu kitaaluma. Ni mtoto wa Mzee Salumu Mshamu na Bi Esha Namalove wa
Mtongwele Chilangala Wilayani Newala Mkoani Mtwara.
Alizaliwa tarehe 01/05/1980
katika kijiji cha Mtongwele Chilangala.
1989 – 1995: Alisoma elimu
yake ya msingi katika shule ya Msingi Mbonde wilaya ya Newala.
1996 – 1999: Alisoma elimu
ya sekondari katika shule ya kutwa Mnyambe Wilaya ya Newala .
2003: Alijiunga na chuo cha
ualimu Bustani Wilayani Kondoa mkoani Dodoma kwa mafunzo ya ualimu ngazi ya
cheti.
2004: Aliajiriwa
Halmashauri ya Wilaya ya Masasi kama Mwalimu na alipangiwa shule ya Msingi
Mbonde ambako anafundisha hadi leo.
2010: Alifanya mtihani wa
kidato cha sita (6) katika shule ya Ndanda kama mwanafunzi wa kujitegemea.
Baada ya matokeo alijiunga na chuo Kikuu cha Waislamu Morogoro ambako alihitimu
na kutunukiwa shahada ya Ualimu (B.A Education) Mwaka 2013.